Akizungumza katika kikao hicho cha dharura cha Jumuiya ya Nchi za Kiarabu mjini Cairo, Misri hapo jana, Gebran Bassil alisema uamuzi huo wa Trump uinapaswa kukabiliwa na vikwazo vya pande zote dhidi ya Marekani.
Aliongeza kuwa nchi wanachama wa jumuiya hiyo zinafaa kuichukulia Marekani hatua za kidiplomasia, kisiasa na kisha vikwazo vya kiuchumi na kifedha.
Bassil amesema anatumai mgogoro huo ulioibuliwa na Trump utaziamsha kutoka usingizini nchi za Kiarabu na kuzileta pamoja, akisisitiza kuwa iwapo zitaifumbia macho kadhia hiyo, basi historia haitawasamehe.
Kwa upande wake, Ahmed Aboul-Gheit, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ameuambia mkutano huo kuwa, kuna udharura wa mataifa yote duniani kulitambua taifa huru la Palestina, mji mkuu wake ukiwa Quds Tukufu.
Naye Riyadh al-Maliki, Waziri wa Mambo wa Nje wa Palestina amezitaka nchi wanachama wa Arab League ziwaagize wajumbe wao katika Umoja wa Mataifa kuwasilisha kwa Baraza la Usalama la umoja huo, rasimu ya azimio la kukabili hatua hiyo ya kichokozi ya Trump, inayoendelea kulaaniwa na aghalabu ya mataifa ya dunia n ahata waitifaki wakuu wa Marekani kama vile Uingereza, Ujerumani na Ufaransa pia wamepiga vikali uamuzi huo.