IQNA

Kiongozi Muadhamu atoa wito kwa India iwatendee uadilifu watu wa Kashmir

11:34 - August 22, 2019
Habari ID: 3472095
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema anasikitishwa na hali waliyonayo Waislamu wa eneo la Kashmir nchini India.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo Jumatano mjini Tehran wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Rais Hassan Rouhani na baraza lake la mawaziri na kueleza kuwa: "Sisi tuna uhusiano mzuri na serikali ya India lakini tunataraji kuona serikali ya India ikitekeleza siasa za kiadilifu mkabala na raia wema wa Kashmir lakini pamoja na hayo tunataraji kuwa  itawatendea uadilifu Wakashmir." Kiongozi Muadhamu amekumbusha kuwa, hali ya mambo ya sasa katika eneo la Kashmir na hitilafu zilizopo baina ya India na Pakistan kuhusiana na kadhia hiyo kuwa ni matokeo ya hatua za Uingereza khabithi wakati wa kuondoka Bara Hindi na kuongeza kuwa: "Waingereza kwa makusudi wameacha jeraha hilo katika eneo ili kuendeleza mapigano huko Kashmir."

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Kiongozi Muadhamu ameashiria maendeleo na kuongezeka uwezo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika nyanja za kisiasa, kiulinzi na kiuchumi na kusisitiza kuwa: Adui hathubutu kufanya upuuzi wowote; na ni wazi kuwa katika miaka 40 ya pili hali ya Jamhuri ya Kiislamu itakuwa bora zaidi kuliko miaka 40 ya awali; na hali ya maadui itakuwa mbaya zaidi.

Marekani, Ulaya na hata Sovieti ya zamani katika kipindi hiki cha miaka 40 zilifanya kila jambo waliloweza dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hata hivyo hazikufanikiwa. Ayatullah Khamenei aidha ameashiria suala la uchumi na akasema ubadilishaji wa mafuta ghafi ili kuzalisha bidhaa mbalimbali ni njia kuu ambayo itasaidia kuacha kutegemea uuzaji nje mafuta. Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa kama ambavyo imeelezwa mara kadhaa, mbali na bidhaa zilizopo sasa kama gesi na petroli, katika siku za usoni tutaweza kubuni na kuzalisha bidhaa nyingine ambazo thamani yake itakuwa kubwa mara kadhaa kulilo ile ya mafuta ghafi kwa kustafidi na wasomi na wanaviwanda.

3836549

captcha