IQNA

Rais wa UAE aaga dunia akiwa na umri wa miaka 73

22:10 - May 13, 2022
Habari ID: 3475246
TEHRAN (IQNA)- Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) au Imarati, Sheikh Khalifa bin Zayed Al Nahyan amefariki dunia.

Shirika rasmi la habari la UAE, WAM . limeripoti habari hiyo leo kupitia ujumbe wa twitter na kuongeza kuwa "Wizara ya Masuala ya Urais imetangaza kwamba, kutakuwa na siku 40 za maombolezo rasmi, ambapo bendera zitapepea nusu mlingoti na siku tatu za kufungwa shughuli zote katika mawizara, vyombo rasmi vya serikali kuu na za ndani pamoja na sekta za binafsi.

Sheikh Khalifa, aliyeaga dunia akiwa na umri wa miaka 73, alikuwa akionekana kwa nadra hadharani tangu alipopata maradhi ya kiharusi mwaka 2014, huku ndugu yake, mrithi wa ufalme wa Abu Dhabi Mohammed bin Zayed, maarufu kama MBZ akionekana kuwa ndiye mtawala halisi na mpitishaji mkuu wa maamuzi katika sera kuu za nje, ikiwemo hatua ya Umoj huo wa Falme za Kiarabu kujiunga katika vita vinavyoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya Yemen na kushiriki katika mpango wa kuiwekea vikwazo nchi jirani ya Qatar katika miaka ya karibuni.

Kwa mujibu wa katiba ya UAE, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, mtawala wa Dubai ambaye ndiye Makamu wa Rais na Waziri Mkuu, atakaimu cheo cha urais hadi pale Baraza la Shirikisho linaloshirikisha watawala wa falme saba za UAE litakapokutana ndani ya kipindi cha siku 30 kumchagua rais mpya.

3478879

Kishikizo: uae
captcha